Followers

Tuesday, 21 October 2014

SIASA ZA MISS TANZANIA

Siasa zisiingizwe Miss Tanzania

OKTOBA 11 mwaka huu zilifanyika fainali za Shindano la Urembo Tanzania ‘Miss Tanzania’ na kushirikisha warembo kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini.

Katika fainali hizo, mrembo Sitti Mtemvu alitangazwa kuwa ndiye Miss Tanzania 2014 na kukata tiketi ya kuipeperusha bendera ya Tanzania katika mashindano ya Dunia ‘Miss World’.

Lakini, tangu Sitti ambaye ni mtoto wa Mbunge wa Temeke jijini Dar es Salaam, Abbas Mtemvu atangazwe mshindi, wadau mbalimbali wa masuala ya urembo walianza kupinga ushindi wake wakidai kuna upendeleo.

Mengi yamesemwa kuhusiana na ushindi huo ikiwemo madai ya kuzidi umri uliopangwa kwa washiriki, ambao ni kuanzia miaka 18 na usizidi 24.

Katika kutetea hoja zao, wadau hao wameanika katika mitandao ya kijamii pasi yake ya kusafiria na leseni ya gari zikionyesha ana miaka 25.

Pia wanadai siku ya shindano mrembo huyo alikiuka maelekezo baada ya kuchagua lugha ya kiingereza katika kujibu swali lakini baadaye akatumia Kifaransa.

Jinsi malalamiko hayo yalivyozidi, Kamati ya Miss Tanzania imejitokeza kumtetea na kudai wao wanatambua kuwa ana miaka 23 na alishinda kwa vigezo stahiki.

Lakini kubwa lililotusukuma Tanzania Daima kuandika tahariri hii, jinsi baba mzazi wa Sitti, kulihusisha na masuala ya kisiasa.

Mtemvu akiwa katika majukumu yake ya kuwatumia wananchi wa jimbo lake mwishoni mwa wiki iliyopita, aliwatuhumu watu kadhaa kuwa ndio wanaoliratibu kwa maslahi ya kisiasa.

Mbunge alikaririwa kuwa, jambo hilo linaratibiwa mahasimu wake kisiasa ambao wana nia ya kugombea nafasi hiyo mwakani.

Sisi Tanzania Daima hatuungani na utetezi huu na kama hakuna ushahidi wa kumtetea Sitti, siasa zisitumike kama kichaka.

Mtemvu kama baba mzazi, tulitegemea aanike ukweli ikiwamo utata wa umri wa mwanaye na si kukimbilia kuwa ni masuala ya kisiasa.

Hoja zijibiwe kwa hoja na si vinginevyo. Familia ya Mtemvu na Kamati ya Miss Tanzania, wajipange kwa hoja na ushahidi wa uhakika ili kurejesha imani kwa jamii ambayo ina ukakasi na ushindi wa mrembo huyo na si kutumia siasa kichaka cha kuzima hoja za wanaodai kuna ulakini katika ushindi wa Sitti.

0 comments: